Header Ads

KUPATA KIBALI KWA BWANA Na Pastor Paul William



Nawasalimu kwa jina lipitalo kila jina,Jina la Yesu Kristo aliyekufa na kufufuka. 

Ni matumaini yangu kuwa wewe unayesoma ujumbe huu Bwana amekuhifadhi mpaka kufikia leo zikiwa zimebaki siku chache kumaliza mwaka 2021 nakutamkia heri na baraka tele Mungu akuvushe na 2022 uwe mwaka wa neema kwako na kufutwa machozi katika jina la Yesu.

Sasa kwa ruhusa yako naomba sasa nianze kuelezea ujumbe huu ambao Bwana amenipa kwa ajili yako na bila shaka utakuwa ujumbe utakaokutoa sehemu moja kwenda nyingine kihuduma,maisha,biashara n.k

Kumekuwa na minong'ono mingi kutoka kwa baadhi ya watu wakidai kuwa siku hizi hakuna wahubiri wa neno la Mungu ila kuna wachumia tumbo tu,watu wasio na uchungu na roho za watu bali wana uchungu na pesa zilizo katika waleti,mikoba na mifuko ya watu. Jambo hili kwa muda mrefu limenipa kutafakari sana na limeumiza moyo wangu, lakini je,ukweli ni upi?

Kwa sehemu naweza kukubaliana na watu wanaosema hivyo kutokana na ukweli usiopingika kuwa siku hizi wapo wengi wajiitao watumishi wa Mungu hali ya kuwa sio wa Mungu bali wamejiingiza kwa siri,"Kwa maana kuna watu waliojiingiza kwa siri,watu walioandikiwa tangu zamani hukumu hii,makafiri,wabadilio neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi....." Yuda 1:4

Watu wa namna hii kamwe hawawezi kufundisha iliyo kweli kwani wakifanya hivyo wanajua fika kabisa kazi yao ya kujikusanyia kipato itakuwa ngumu kwani watu wengi hawapendi kuambiwa ukweli na ikitokea hivyo wanahama kanisa. Mtu ni mwizi,mtoa rushwa,mpokea rushwa amepata mali kwa njia zisizo halali lakini anataka akija katika nyumba ya ibaada aambiwe "pokea baraka" sasa wahubiri wengi wa kileo wanajua udhaifu huo na wameutumia vilivyo.

Wengine wanahangaika kiuchumi na wakija kanisani wanaambiwa toa ubarikiwe,panda mbegu,mara toa sadaka ya kuteketezwa ili mambo yako yafunguke,lakini cha ajabu mtu huyu tangu afanye hivyo hizo baraka alizoahidiwa hajawahi kuzipata badala yake ugumu wa maisha uko palepale na mhubiri anazidi kunona,ndipo wengi wanahitimisha kwa kusema wahubiri wote si wakweli,hakuna miujiza wala baraka kupitia maombi.

Ndugu msomaji wangu,baraka zipo tele kwa watoaji kama Biblia isemavyo "Ni heri kutoa kuliko kupokea" Mdo 20: 34-35 ndivyo ilivyo maana Mungu si mwanadamu hata aseme uongo Hesabu 23:19 Lakini pamoja na ahadi hizo kuna mambo ya kuzingatia kama wasemavyo watu wa mitandao "vigezo na masharti kuzingatiwa"

Tunachopaswa kukifanya wahubiri wenzangu ni kuwaeleza watu kweli juu ya utoaji,maana Mungu si hakimu wa kidunia kwamba unaweza kumhonga na akapindisha sheria la hasha.! Wengi tumefundisha hivyo "toa ubarikiwe" hii imepelekea wengi kumfanya Mungu kama SACCOS ya kuweka na kukopa,mpendwa Mungu si mfanyabiashara ama taasisi ya uwekezaji kwani " fedha na dhahabu ni mali yake" Hagai 2:8 anachokitaka toka kwa mtu ni usafi wa moyo," Heri wenye moyo safi maana hao watamwona Mungu' Mathayo 5:8

Hayo maneno "watamwona Mungu" si tu pale watakapofika mbinguni bali pia katika maisha yao ya hapa duniani,kumbuka Yesu alivyosema " mara mia duniani kisha uzima wa milele" kumbe Mungu unaanza kumwona katika maisha yako kawaida,inawezekana ulishawahi kusikia mtu akisema nimemwona Mungu baada ya maombi haya,nimemwona Mungu kwenye kazi au biashara yangu, hii inamaanisha Mungu amemtendea jambo.

Sasa ili Mungu aonekane kwako anachokitaka sio kiasi fulani cha pesa kumbuka Yesu alisema "Nataka rehema wala si sadaka" Mt 9:13 hapa Yesu hamaanishi tusitoe sadaka ila kipindi hicho Wayahudi walizoea kila baada ya muda fulani walipeleka kwa kuhani sadaka ya dhambi,kwa hiyo mtu alifanya atakavyo maadamu anajua muda utafika nipeleke sadaka ya dhambi nami nitakuwa safi sasa hii haina tofauti na hongo ama rushwa na Mungu wetu hayupo kama tulivyo wanadamu.

Anachokiangalia MUNGU kwanza si sadaka bali humtazama mtoaji kwanza yukoje ndani "  “Nawe Solomoni mwanangu, umjue Mungu wa baba yako, na umtumikie kwa moyo wako wote na kwa nia thabiti; yeye Mwenyezi-Mungu huchunguza mioyo na anafahamu mipango na fikira za binadamu. Ukimtafuta yeye, utamwona; lakini ukimwacha, atakutupilia mbali milele. 1 Nyakati 28:9

Sasa unaona aya hiyo...huchunguza mioyo... wanadamu hatujuani kwa undani lakini yeye muumba anatujua,mfano mtu anakuja kutoa sadaka/fungu la kumi n.k halafu mchungaji namtamkia ubarikiwe wakati mtu huyu jana tu alikuwa nyumba ya wageni na mke wa mtu,au wakati mwingine mtu anatoa sadaka na haelewani na wazazi wake au ana kinyongo moyoni kuna mtu hajamsamehe nataka nikuambie mtu wa namna hii hata kama atauza mashamba aje kutoa sadaka na mchungaji ukamtamkia baraka ni sawa na kujaza maji katika tenga la nyanya.

Katika kitabu cha Mwanzo 4:4-5 kuna maneno yasemayo "Habili naye akaleta wazao wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona za wanyama. BWANA akamtakabali Habili na sadaka yake; bali Kaini hakumtakabal" neno kutakabali ni kukubali/kukubaliwa/kupata kibali

Unaona Mungu anaanza kwanza kumkubali mtu kabla hajaikubali sadaka aliyoileta,hapa wahubiri wengi tumepotosha kwa muda mrefu kuwa kaini alitoa vibaya,hakutoa vinono jambo ambalo si kweli na haijaandikwa hivyo bali tunatumia kauli hiyo ili kuwafanya watu watoe sadaka nzuri maisha yetu yaende,nikuulize ulitaka kaini atoe nini wakati hiyo ndiyo ilikuwa kazi yake(kulima) na mdogo wake alikuwa mfugaji hivyo alipeleka kwa Mungu kutokana na kile anachokifanya,sasa tofauti yao ilikuwa nini? jibu ni MOYO. Mmoja alikuwa safi na mwingine hakuwa safi mbele za Bwana.

Yesu mwenyewe alisema kwa habari ya sadaka katika Mathayo 5:23-24

"Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako"

Hivyo ili upate kibali katika suala la utoaji huna budi kuhakikisha moyo wako ni safi na ukifanya hivyo utaziona baraka za Mungu zikimiminika maishani mwako kwani " Sadaka ya mtu mbaya ni chukizo kwa Bwana" Mithali 15:8

Mungu akubariki kwa maombi na ushauri nipigie kupitia +255742133926



No comments