Header Ads

SAMATTA: NILIKUWA NALALA UWANJANI WAKATI NATAFUTA NAMBA YA KUDUMU SIMBA.

Mbwana Samatta 2
Hakuna ubishi kwamba kila mafanikio yanakuja kwa bidii, kujituma, kujitoa, nidhamu na vitu vingine vingi sana tofauti na baadhi ya watu wanavyofikiria kwamba unaweza ukapata mafanikio kwa njia ya mkato bila kupambana.
Mafanikio aliyonayo leo Super Star wa soka la Bongo Mbwana Samatta hayajaja hivihivi ‘kimagumashi’, jamaa alikuwa anatoka nyumbani saa 10:30 alfajiri ili awahi mazoezi ambayo yalikuwa yanaanza saa 1:00 asubuhi.
Samatta anasema ilimbidi awahi kutoka nyumbani kwasababu alikuwa hana gari na ili asichelewe mazozi, alilazimika kutoka nyumbani muda huo kila siku ili kukwepa adha ya usafiri wa Mbagala kwani angetoka muda mwingine zaidi ya huo basi ni lazima angechelewa mazoezi.
Kwasababu muda huo kunakuwa na magari mengi lakini pia kunakuwa hakuna foleni alikuwa anawahi sana kufika uwanjani. Alipokuwa akifika uwanjani alikuwa analala na kila siku kocha wa Simba alikuwa anamkuta Samatta uwanjani hali iliyopelekea kocha wa kipindi hicho Patrick Phiri kutafuta njia ya kumpa nafasi Samatta kwenye kikosi cha kwanza kutokana na jitihada alizokuwa akizionesha.
Kocha yeye alikuwa anafika uwanjani saa 12:00 asubuhi kwa ajili ya mazoezi, lakini alikuwa ananikuta mimi nimelala kwenye majukwaa. Nilikuwa nafika saa 11:00 asubuhi halafu nalala kwenye majukwaa.
Hii ilitokana na aina ya usafiri wa Mbagala ambako nilikuwa naishi mimi. Kipindi hicho nilikuwa bado sijapewa gari, mazoezi yalikuwa yanaanza saa 1:00 asubuhi, usafiri wa daladala kutoka Mbagala ukisema utoke saa 12 asubuhi tayari umeshafeli. Kwahiyo mimi nilichokuwa nakifanya, nilikuwa natoka saa 10:30 alfajiri muda huo magari yanakuwa si ya kugombea na barabarani kunakuwa hakuna foleni.
Nikuwa nafika uwanja wa taifa (shamba la bibi) saa 11 asubuhi mlinzi ananifungulia nakaa kwenye majukwaa hadi napitiwa na usingizi. Mwalimu akija ananikuta na ilikuwa hivyo karibu kila siku kabla sijapata gari. Mwalimu akawa ananiona akaanza kubadilika kwa kuniona kila siku nawahi na yeye akija ananikuta uwanjani nimelala kwenye majukwaa hata leo ukimuuliza Patrick Phiri atakutolea mfano kuhusu hili suala.
Baada ya kuwa nimeshaanza kufanya vizuri na Simba akawa anautoa mfano ule kwa wachezaji vijana ambao walikuwa wanakuja.
Kabla ya mechi kati ya Simba na TP Mazembe alisema (Phiri), najua katika timu hii kuna mchezaji mmoja au wachezaji wawili leo ndiyo itakuwa siku yao ya mwisho kucheza Simba. Baada ya mechi huenda wakanunuliwa na Mazembe au wakanunuliwa na klabu nyingine lakini nauhakika mechi hii mchezaji mmoja au wawili watacheza Simba kwa mara ya mwisho.
Sijui alimlenga nani, sisemi kwamba alinilenga mimi ila aliyasema hayo maneno. Bahati nzuri ikawa hivyo ikatokea kwangu na kwa Ochan, kuna kipindi nilikuwa nawasiliana na Phiri alikuwa ananiambia alikuwa inspired na jitihada zangu na ikamfanya abadilishe baadhi ya mambo. “Niliona kama ulikuwa unateseka kwa ajili ya kitu flani nikaamua nikupe nafasi”, Samatta anasema hayo yalikuwa maneno ya Patrick Phiri.
Huu ni mwazo tu wa simulizi ya ‘Safari Ndefu ya Samatta kutoka Mbagala kuelekea Ulaya’ ungana nami tena kesho kwenye mwendelezo wa simulizi hii ambapo kesho itaanzia namna Samatta alivyosajiliwa na TP Mazembe. Ilikuwaje, siku ya kwanza akiwa Mazembe na mengine kibao…usikose
Cheki video hapa wakati Samatta akieleza namna alivyokuwa akipambana kupata namba ya kudumu kwenye kikosi cha Simba SC hadi kufikia kulala uwanjani.

No comments