Header Ads

Wafanyabiashara mtandao wa Trevo walipwa Sh3.5 bil

Mkurugenzi wa kampuni ya Trevo nchini, David Kagoro 

Dar es Salaam. Zaidi ya wafanyabiashara 10,000 nchini wanaojihusisha na biashara ya mtandao ya dawa lishe ya Trevo wamelipwa Sh3.5 bilioni za kamisheni kwa kazi wanazofanya.

Mkurugenzi wa kampuni hiyo nchini, David Kagoro alisema kiasi hicho kilitolewa ndani ya miezi 17 ya awali kwa awamu tangu walipoanza kufanya biashara hiyo mwishoni mwaka juzi hadi Aprili mwaka huu.

Kagoro alisema fedha hizo ziliwasaidia wafanyabiashara waliomo katika mtandao wa bidhaa zao kwa kukuza mitaji, kuwaongezea uhuru wa kifedha na kuchangia uchumi wa Taifa kwa kutoa kodi ya zuio na kuwapatia wananchi ajira.

Trevo ni dawalishe iliyo katika kimiminika ambayo mfumo wake wa biashara hufanywa kwa wafanyabiashara kutengeneza mitandao na wateja wapya na kulipwa kamisheni kama zilivyo bidhaa za kampuni za Forever Living na GNLD.

Kagoro alisema tangu kampuni hiyo ya Kimarekani iingie nchini mwishoni mwa 2014, wamefikisha wafanyabiashara 12,000 kwenye mtandao ambao anaamini wataongezeka siku hadi siku.

Ofisa Mtendaji Mkuu na mwanzilishi wa kampuni hiyo, Mark Stevens alisema lengo la biashara yake ni kuwasaidia Watanzania kupata uhuru wa kifedha kwa kujikita kufanya ujasiriamali wa kimtandao kama wanavyofanya katika uuzaji wa bidhaa zingine.

“Hadi sasa tumeona Watanzania wengi wakihamasika kutumia fursa ya biashara hii na wamekuwa viongozi wazuri katika mitandao wanayoanzisha,” alisema Stevens.

Alipoulizwa kuhusu ufanisi wa dawalishe hiyo yenye virutubisho 174, Samweli Mtullu, Daktari wa Hospitali ya Lubombo mkoani Tanga, alisema hadi sasa watumiaji wameonyesha kupata ahueni mara watumiapo.

Mmoja wa wafanyabiashara waliopo kwenye mtandao, Wisley Usiri alisema alianza kufanya biashara hiyo mwaka juzi. Alisema licha ya kukumbana na changamoto kadhaa, amefanikiwa kujiingizia Sh5 milioni kila mwezi.

No comments