Header Ads

TCRA yazipiga faini E FM, Kahama FM.


                                                          Mwenyekiti wa Kamati ya Maandili ya TCRA, Margaret Munyagi
MAMLAKA ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imevipa onyo na kuvipiga faini vituo viwili vya redio kutokana na kukiuka maadili ya utangazaji.
Vituo hivyo ni Entertainment FM (E FM) cha Dar es Salaam na Kahama FM Stereo ya Kahama, mkoani Shinyanga.
Akitoa maamuzi yaliyofikiwa na Kamati ya Maandili ya TCRA, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Margaret Munyagi, alisema vituo hivyo vimebainika kukiuka sheria na kanuni za utangazaji.
Amevitaka vewe na usimamizi mzuri wa vipindi vyao.
Munyagi alisema kamati yake imekipa onyo kali na faini ya sh milioni moja kituo cha Efm na endapo kitarudia, hatua kali zaidi zitachukuliwa.
Alisema Januari 4 mwaka huu, kituo hicho katika kipindi cha ‘Joto la Asubuhi’ katika kipengele cha ‘Sala ya Siku’, kilichorushwa kati ya saa 1 hadi 3 asubuhi, Mtangazaji alihamasisha vitendo vya wizi, ngono na uchochezi wa kidini.
Katika utetezi wake, Mkurugenzi wa kituo hicho, Dennis Busulwa pamoja na kukiri kufanya kosa, alisema kituo chake kilijibebesha mzigo mzito wakati bado ni wachanga katika utangazaji na kutokana na kosa hilo waliamua kukiondoa kipengele hicho.
Kwa upande wa Kahama FM Stereo, Munyagi alisema kituo hicho kimepewa onyo kali, kutozwa faini ya Sh 200,000 na endapo watajirudia watapewa adhabu kali.
Januari Mosi mwaka huu, kupitia kipindi cha ‘Wanawake’ kilichorushwa hewani kati ya saa 3 asubuhi na saa sita mchana, mtangazaji alimhoji mwanamke aliyekuwa akifanya biashara ya kujiuza.
“Mahojiano hayo yalijikita katika kuelezea jinsi biashara ya kujiuza inavyofanyika katika mji wa Kahama kwa kubainisha changamoto na faida ambazo wafanyabiashara hiyo wanazipata. “Kuwepo kwa majadiliano haya katika muda wa asubuhi kunaweza kuchochea tabia mbaya kwa watoto kuiga vitendo vya ufanyaji ngono,” alisema.
Katika utetezi wake, Meneja wa Kahama FM Stereo, Marco Mipawa, alikiri kikiuka sheria na kanuni za utangazaji na kuahidi kwamba tatizo hilo halitajirudia tena.

 CREDIT:HABARI LEO

No comments