Header Ads

Steven Wasira Awekewa Pingamizi Tena


Wapiga kura wa Bunda Mjini waliowasilisha maombi ya kuruhusiwa kukata rufaa nje ya muda, kupinga matokeo ya uchaguzi yaliyompa ushindi Ester Bulaya dhidi ya Steven Wasira, wamekumbana na kigingi kingine cha pingamizi.

Maombi hayo namba 25 ya mwaka 2016 yaliwasilishwa na wapiga kura Magambo Masato na wenzake watatu, wakiiomba mahakama hiyo iwaruhusu kukata rufaa nje ya muda baada ya kutupiliwa mbali na mahakama kuu.

Pingamizi hilo liliwasilishwa jana na wakili wa wajibu maombi wa pili na wa tatu, Paschal Malulu akiiomba mahakama kutupilia mbali maombi hayo kwa kuwa kiapo kilichoambatanishwa ni batili kwa kuwa aliyeapa ni tofauti na aliyethibitisha.

“Haya makosa yaliyofanyika ni makubwa mno, kiasi cha kutokurekebishika, kwa sababu kiapo kimethibitishwa na wakili Constatine Mutalemwa huku aliyeapa ni wakili James Kahangwa,” alidai Malulu.

Alidai kiapo hicho kimekosa nguvu kisheria kwa mujibu wa sheria Na. 19 (1) (2), ni lazima kiwe na mambo ambayo mtu anaweza kuyathibitisha au kuyasimamia, hivyo hii sheria imekiukwa, kwa lugha nyingine kiapo kimekosa uthibitisho.

Malulu alidai kuwa kuna sheria inayosimamia kiapo wala siyo Katiba kwa ujumla wake, kama alivyoitaja Mutalemwa.

Jaji anayesikiliza shauri hilo, Rose Ebrahim aliahirisha shauri hilo hadi Machi 14, mwaka huu atakapolitolea maamuzi pingamizi hilo.

No comments