Header Ads

Meya wa Zamani wa Ilemela Henry Matata Afikishwa Mahakamani Kwa Matumizi Mabaya ya Ofisi


TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Mwanza, imemfikisha mahakamani aliyekuwa Meya wa Manispaa ya Ilemela, Henry Matata (63) na wenzake wawili wakikabiliwa na mashitaka ya kutumia vibaya madaraka.

Washitakiwa wengine katika kesi hiyo waliofikishwa jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Wilaya ya Nyamagana ni aliyekuwa Mhandisi wa Manispaa ya Ilemela, Justine Lukaza (42) na mfanyabiashara Hemedi Hamad (54).

Mwendesha Mashitaka wa Takukuru, Mwema Mella, alidai mbele ya hakimu Greyson Sumaye kwamba kati ya Juni mosi na Julai 31, mwaka 2014, washitakiwa hao walitumia vibaya madaraka kwa kutoa zabuni ya kutoza ushuru katika Kituo cha Mabasi cha Buzuruga kinyume cha utaratibu.

Alifafanua kuwa makosa waliofanya ni kinyume na kifungu cha 31 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa mamba 11/2007 na pia walikiuka sheria ya manunuzi ya umma namba 7/2011

 Wakati kesi hiyo inafikishwa mahakamani jana, mshitakiwa Lukaza hakuwepo, hatua iliyomfanya Mwendesha Mashitaka kuomba mahakama hati ya kumkamata.

Hakimu aliridhia ombi hilo na kesi hiyo ilioahirishwa hadi Machi 29 mwaka huu. Washitakiwa wawili waliokuwepo mahakamani walikana mashitaka hayo na wako nje baada ya kutimiza masharti ya dhamana.

No comments