Header Ads

UMUHIMU WA VITAMINI D.

Vitamini D ni miongoni mwa vitamini zinazochanganyika na mafuta. Nyingine katika kundi hili ni A,E na K. Vitamini D maarufu kama “vitamini ya jua” hujulikana kitaalamu pia kama (calciferol)(Ergocalciferol)  Vitamini D3 (Cholecacliferol).

Vitamini D ni aina ambayo hupatikana katika aina chache za vyakula, lakini hupatikana pia kama virutubisho vya kutengeneza viwandani,au vyakula ambavyo huongezewa Vitamini D. Vyakula vyenye Vitamini D ni kama mayai, samaki, mafuta ya samaki, maziwa ya mama na maziwa ya wanyama. Mwili pia una uwezo wa kutengeneza vitamini hii na kujitosheleza kwa kupitia  nishati ya jua. Kuota jua hasa nyakati za asubuhi huiwezesha miili yetu kutengeneza Vitamini D.

Vitamini hii inahitajika mwilini kwa ajili ya kurekebisha madini kalshamu (calcium) na phosphorasi (phosphorus) mwilini. Vitamini hii husaidi kusharabiwa mwilini kwa madini ya kalshamu na kuimarisha mifupa na meno. Kuota jua ni njia rahisi ya watu kujitengenezea vitamini D. Jua hasa la asubuhi linapokupata katika uso, mikono na miguu angalau mara 2 mpaka 4 kwa wiki itasababisha ngozi yako kutengeneza Vitamini D ya kutosha.

Ingawa Vitamini hii hupatikana kwa kuota jua, watu hupata upungufu wa vitamini D kuliko vile ungeweza kutegemea. Wale wasiopata jua la kutosha wako katika hatari ya upungufu wa vitamini D. Wazee wasiojiweza huwa ni waanga wakubwa wa upungufu huu, hii ni kwa sababu hukaa ndani muda mrefu bila ngozi zao kupata mnururisho wa jua. Twaweza kusaidia kundi hili la wazee wasiojiweza kwa kuwatoa nje kuota jua ili kujitengenezea Vitamini D. Pia wale wanaotumia mara kwa mara losheni za kuzuia mionzi mikali ya jua waweza kuwa katika hatari ya upungufu. Katika nchi zenye joto na jua kali watu hujifunika uso, mikono hata miguu kuepuka kuungua na jua au kukaa ndani hata jua litakapozama ili waendelee na shughuli zao za kila siku.

Upungufu wa Vitamini D huambatana na kukosa kupata jua la kutosha. Upungufu wa vitamini D umekuwa tatizo kubwa kwa wazee wasiojiweza, na kawaida kwa watoto na watu wazima. Upungufu huu hupelekea mtu kupata magonjwa yafuatayo:-


  • Rickets- Ni ugonjwa wa watoto ambao hudumaza ukuaji wa mtoto na huambatana na mifupa ambayo ni laini na dhaifu, mifupa ambayo haikujengeka vizuri, mtoto kuwa na uzito mdogo kulinganisha na umri pia kupinda kwa mifupa ambayo huzidiwa na uzito wa mwili (matege).Udhaifu wa mifupa hutokana na kutosharabiwa kwa madini ya kalshamu pia husababisha kushindwa kuziba kwa utosi wa mtoto(failure of the fontanelle to close). Matatizo haya ya upungufu ni makubwa zaidi hasa katika nchi zenye kipato cha chini ukilinganisha na nchi zilizoendelea.
  • Osteomalacia- Huu ni ugonjwa ambao huwapata watu wazima wenye upungufu wa Vitamini D. Ugonjwa huu hupelekea mifupa kuwa dhaifu,ambapo hupelekea kupinda kwa mifupa ya uti wa mgongo, udhaifu wa misuli, maumivu ya misuli na kupinda  miguu kutokana na kuelemewa na uzito wa mwili. Vitamini D husaidia kusharabiwa kwa kalshamu kwenye damu na madini haya hupelekwa kwenye mifupa.Kwa hiyo pungufu wa vitamini hii hupelekea kalshamu iliyoko kwenye mifupa kwenda kwenye damu kwa ajili ya kazi nyingine za mwili kama utendaji kazi wa misuli.

No comments