Header Ads

Kumbukumbu ya miaka 16 kifo cha Baba wa Taifa Hayati J.K Nyerere.

Julius Kambarage Nyerere alizaliwa mwaka 1922 katika kijiji cha Butiama, wilaya ya Musoma, mkoa wa Mara, Tanzania (wakati ule: Tanganyika).
Alikuwa mmojawapo kati watoto 26 wa Nyerere Burito, chifu wa kabila la Wazanaki.
Alipokuwa mtoto Nyerere alichunga mifugo ya baba yake; katika umri wa miaka 12 aliingia shule akitembea kilomita 30 hadi Musoma.
Baada ya kumaliza shule ya msingi aliendelea kusomea shule ya wamisionari Wakatoliki huko Tabora. Katika umri wa miaka 20 alibatizwa akawa Mkristo Mkatoliki hadi mwisho wa maisha yake.
Mapadri wakiona akili yake kubwa walimsaidia kusomea ualimu huko Makerere, Kampala, Uganda kuanzia mwaka 1943 hadi 1945.
Akiwa Makerere alianzisha tawi la Umoja wa Wanafunzi Watanganyika, pia alijihusisha na tawi la Tanganyika African Association (TAA).
Baada ya kumaliza masomo ya ualimu alirudi Tabora akifundisha shule ya St.Mary. Mwaka 1949 alipata skolashipu ya kwenda kusoma kwenye Chuo Kikuu cha Edinburgh, Uskoti, Ufalme wa Muungano, akapata M.A. ya historia na uchumi (alikuwa Mtanganyika wa kwanza kusoma katika chuo kikuu cha Uingereza na wa pili kupata shahada ya elimu ya juu nje ya Tanganyika).
Aliporejea kutoka masomoni, alifundisha Historia, Kiingereza na Kiswahili katika shule ya St. Francis iliyo karibu na Dar es Salaam.
Mwaka 1953 alichaguliwa kuwa rais wa chama cha Tanganyika African Association (TAA), chama ambacho alikisaidia kukijenga alipokuwa mwanafunzi katika chuo kikuu cha Makerere.
Mwaka 1954 alibadilisha jina la chama cha TAA kwenda chama cha Tanganyika African National Union (TANU), ambacho pia kilikuwa cha kisiasa zaidi kuliko TAA.
Ndani ya mwaka mmoja chama cha TANU kikawa tayari chama cha siasa kinachoongoza nchini Tanganyika.
Uwezo wa Nyerere uliwashtua viongozi wa kikoloni akalazimika kuchagua kati ya siasa na kazi ya ualimu.
Nyerere alisikika akijisemea kuwa mwalimu kwa kuchagua na mwanasiasa kwa bahati mbaya.Alijiuzulu ualimu na kuzunguka nchi nzima ya Tanganyika kuzungumza na watu wa kawaida na machifu ili kuleta umoja katika kupigania uhuru.
Pia alizungumza kwa niaba ya TANU katika Trusteeship Council na Fourth Committee ya Umoja wa Mataifa (UN) huko New York.
Uwezo wake wa kuongea na wa kuunganisha watu ulimwezesha kufanikisha Tanganyika kupata uhuru bila umwagaji wa damu.
Ushirikiano mzuri aliouonyesha aliyekuwa gavana wa wakati huo, Richard Turnbull, ulisaidia pia kuharakisha upatikanaji wa uhuru.
Nyerere aliingia katika bunge la kikoloni mwaka 1958 na kuchaguliwa kuwa waziri mkuu mwaka 1960.
Mwaka 1961 Tanganyika ilipata uhuru wake na tarehe 9 Desemba 1961 Nyerere alichaguliwa kuwa waziri mkuu wa Tanganyika huru; mwaka mmoja baadaye akawa rais wa kwanza wa Jamhuri ya Tanganyika.
Nyerere alikuwa kiungo muhimu katika muungano wa Tanganyika na Zanzibar kutengeneza Tanzania mara baada ya mapinduzi ya Zanzibar mwaka 1964 yaliyomtoa madarakani sultani wa Zanzibar Jamshid bin Abdullah.
Tarehe 5 Februari 1977 aliongoza chama cha TANU kuungana na chama tawala cha Zanzibar Afro Shirazi Party na kuanzisha chama kipya cha CCM (Chama cha Mapinduzi) akiwa mwenyekiti wake wa kwanza.
Nyerere aliendelea kuongoza taifa hadi 1985 alipomwachia nafasi rais wa pili, Ali Hassan Mwinyi. Aliacha kuongoza Tanzania ikiwa ni mojawapo kati ya nchi maskini zaidi duniani, ingawa yenye huduma za elimu na afya zilizoenea kwa wananchi wengi.
Hata hivyo aliendelea kuongoza CCM hadi mwaka 1990 na kuwa na athari kubwa katika siasa ya Tanzania hadi kifo chake.
Kwa mfano, inasadikika kuwa Nyerere alishawishi uteuzi wa Benjamin W. Mkapa kama mgombea wa urais mwaka 1995, ambaye alichaguliwa kuwa rais kwenye uchaguzi.
Nyerere alikaa muda mwingi kwake Butiama akilima shamba lake. Pamoja na haya alianzisha taasisi yenye jina lake; mwaka 1996 alionekana akiwa mpatanishi wa pande mbalimbali za vita vya wenyewe kwa wenyewe huko Burundi.
Tarehe 14 Oktoba 1999 aliaga dunia katika hospitali ya St Thomas mjini London baada ya kupambana na kansa ya damu.
Sasa ni miaka 16 toka kifo chake, zimebaki takribani siku 10 Tanzania kuingia kwenye Uchaguzi Mkuu wa kupata madiwani, wabunge na Rais.
Huu ni uchaguzi wa pili unafanyika ndani ya Taifa la Tanzania bila uwepo wake.
Kwa mara ya kwanza nchi inakwenda kushuhudia Uchaguzi ambao ni vigumu kutabili hadi sasa kuwa ni nani ataibuka mshindi.
Kama alivyowahi kusema mwaka 1992 wakati nchi inaingia kwenye mfumo wa vyama vingi, alisema mfumo huo utapanua demokrasia huku akibainisha kwamba isiwe ajabu kwa baadhi ya wana CCM kuondoka ndani ya chama hicho na kujiunga upinzani.
Kutoka kwa mawaziri wakuu wastaafu ndani ya CCM na kujiunga upinzani kumeweza kuimarisha zaidi upinzani na kwa mara ya kwanza watanzania wanaenda kushuhudia Uchaguzi usio wa upande mmoja.


No comments