Header Ads

NAPE:KADI ZA CCM ALIZOPEWA LOWASSA NI ZA KUTENGENEZA SIO WANA CCM.


KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, amesema kadi za chama hicho alizokabidhiwa Mgombea wa urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa akiwa Jimbo la Mtama si za kweli, bali mpango uliotengenezwa ili wajipatie umaarufu.

Nape alisema hayo wakati akizungunza na mwandishi mjini Morogoro juzi mara baada ya uzinduzi wa safari ya wasanii wanaounda kundi la NimEs’tuka Hapa kazi tu, linaloongozwa na Aunty Ezekiel na Vincent Kigosi ‘Ray’ uzinduzi uliofanyika kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Kiwanja cha Ndege Manispaa ya Morogoro.

Septemba 23, mwaka huu wakati wa mkutano wa kampeni za Mgombea wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chadema, Lowassa katika kundi la vyama vinne vinavyounda Ukawa ambapo pamoja na mambo mengine, ilidaiwa kadi 3,000 za cha CCM zilipokewa kutoka kwa wanachama na kuunga mkono Ukawa.
Kwa mujibu wa Nape, wakati kadi hizo zinapokelewa na Waziri Mkuu mstaafu aliyehamia Ukawa, Frederick Sumaye, yeye hakuwepo jimboni, bali alikuwa katika shughuli za kampeni za chama chake nje ya mkoa.

“Kadi zote waliozipokea ilitokana na kutengeneza shoo, zote zilikuwa ni mpya hakuna hata moja ya zamani, kwa maana ni mpango mzima wa kutengeneza shoo na Sumaye ndiye alizipokea si mgombea wa urais wa Chadema,” alisema Nape na kuongeza:

 “Hii yote inamaanisha kuwa wananiogopa, binafsi sikuwepo...nilikuwa kwenye kampeni kwa wagombea wa chama changu .”

Kuhusu uzinduzi huo, alisema wasanii hao ni miongoni mwa waliorejea CCM kutoka Ukawa, watazunguka nchi nzima na watapita kila kona ya Tanzania kuwaambia wananchi na vijana nini walichoona wakiwa Ukawa.

Naye Aunty Ezekiel akizungumza mbele ya umati wa wananchi waliokuwepo uwanjani hapo, alisema Ukawa hali si nzuri na kwamba alichambua mchele na pumba ndiyo maana ameamua kurudi CCM.

Alisema mgombea wa urais wa Ukawa, Lowassa amekuwa akihubiri kutaka mabadiliko bila kazi tofauti na mgombea wa urais wa CCM ambaye anahimiza kufanya kazi. 
  
Naye Kigosi ‘Ray’ alisema ameamua kurudi CCM baada ya kuona kuna vitu ambavyo hawavipati kule Ukawa ambavyo vipo ndani ya CCM na alichokiona kikubwa ni siasa za hadaa tupu ‘magumashi.’

No comments