Header Ads

MTOTO WA BWANA SHAMBA AWA KINARA KITAIFA KIDATO CHA SITA.

Ramadhani Gembe 
Wakati Ramadhani Gembe (pichani) anafanya mtihani wa Taifa wa kidato cha sita miezi miwili iliyopita, hakuwahi kufikiri angeshika namba moja kwa ufaulu kitaifa licha ya jitihada zake za kujituma.
Lakini siku zote Mungu hamtupi mja wake. Kama jina lake linavyosadifu mwezi mtukufu unaomalizika siku mbili zijazo, Ramadhani ambaye amehitimu Shule ya Wavulana ya Feza jijini Dar es Salaam, ameibuka mwanafunzi bora nchini kati ya waliofanya mtihani huo wa kujiandaa kwa masomo ya elimu ya juu.
“Nilitegemea ningefaulu lakini siyo kwa kiwango hicho… hii ni ‘surprise’ (shtukizo),” alisema Gembe alipohojiwa na Mwananchi baada ya matokeo ya kidato cha sita kutangazwa na Baraza la Mitihani la Taifa.
“Nawashukuru wazazi, walimu, ndugu na wanafunzi wenzangu kwa kunipa ushirikiano. Nilikuwa nafanya sana ibada hivyo haya matokeo ni juhudi binafsi na majibu ya Mungu,” alisema Ramadhani aliyesoma mchepuo wa fizikia, kemia na baiolojia (PCB).
Historia ya Ramadhani darasani si haba kwani mwaka 2008 alikuwa ni mwanafunzi pekee aliyejiunga na shule ya vipaji maalumu ya Ilboru, Arusha akitokea shule ya Msingi Mombo na alipata daraja la kwanza akiwa na pointi 11 katika matokeo ya kidato cha nne.
“Siku zote kilichonifanya niongeze juhudi katika masomo yangu ni malengo ya baadaye... mimi nataka kuwa daktari wa binadamu hivyo sikutaka kulegalega kusoma. Pia, wazazi wangu pamoja na hali ngumu walijitahidi kunisaidia kimawazo, kirasilimali na kimaadili…naomba na wazazi wengine wawafanyie hivyo watoto wao,” alisema.
Baba azungumza
Nurdin Gembe, ambaye ni mzazi wa Ramadhani, alisema familia imepokea kwa furaha matokeo hayo na kwamba alikuwa akiyategemea kuwa mazuri kutokana historia ya kijana wake katika madarasa ya nyuma.
“Huyu mtoto namlea kawaida japo zamani alikuwa mtundu sana… ilibidi nimpe mafundisho mengi sana ya kidini bila kupoteza ratiba ya kusoma shuleni. Nashukuru kuwa alizingatia na amefika hapo alipofika,” alieleza Gembe ambaye ni bwana shamba kitaaluma.
Mwanafunzi wa tisa
Kwa upande wake Yonazi Senkondo, aliyeshika nafasi ya tisa kitaifa, alisema matokeo hayo ni majibu ya maombi kwa Mungu na juhudi zake kusoma na ushirika na wanafunzi wenzie.
“Siku zote nilikuwa naombea niingie 10 bora, najua leo Mungu amejibu maombi yangu. Nilikuwa nafanya mijadala na wanafunzi wenzangu hasa huyo aliyeshika namba moja. Sishangai yeye kuwa katika ngazi hiyo.MWANANCHI

No comments