Header Ads

GEITA:FAMILIA YASUSIA MAITI

Mkuu wa Mkoa wa Geita Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga akitoa maagizo ya kuhakikisha uchunguzi unafanyika katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa Juu ya wale ambao wamehusika na manyanyaso dhidi ya mgonjwa,ni katika kikao cha sita cha ushauri Mkoani Geita.

Kamati ya ulinzi na usalama Mkoani Geita wa kwanza ni katibu tawala wa wilaya ya Geita Thomas Dibe,wa pili ni kamanda wa mkoa wa Geita Mponjoli Mwabulambo wakisikiliza kwa makini maamuzi juu ya mgonjwa aliyefia kwenye choo hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Geita.

Wajumbe wakifatilia kikao.

Mbunge wa Geita Vijijini Joseph Msukuma akihoji juu ya mgonjwa ambae amenyanyasika na mwisho  kupoteza uhai wake.

Bahati Chihula,ambae ni mtoto wa marehemu akizungumza namna alivyosikitishwa na huduma mbovu alizopatiwa mzazi wake na mwisho wa siku kusababisha kifo chake huku akiweka msimamo wa kutokubeba mwili (maiti)mpaka pale serikali itakapo ingilia kati kuwachukulia hatua za kisheria wale wote ambao wamehusika na kifo cha baba yake kwani ni uzembe wa wauguzi ndio umesababisha Mzee wake kupoteza uhai.

Felix Joseph akielezea kuchukizwa na namna ambavyo walinzi na wauguzi katika hospitali hiyo wamekuwa na majibu mabaya kwa watu wanaokuja kuwasalimia ndugu zao na wagonjwa pia hali ambayo imekuwa ikiwanyima amani wagonjwa na wale ambao wanakuwa wakiwauguza hosptalini hapo.



Familia  yagoma  kuchukua mwili wa marehemu  wa mzazi wao (maiti) kwa  kile kinachodaiwa wauguzi wa hospitali teule ya rufaa ya mkoa  wa Geita kuwa na majibu  machafu  kwa wagonjwa.

Akizungumza na  mtandao huu  katika mazingira ya hospitali hiyo mmoja kati ya wanafamilia ambae  amefiwa na baba yake mzazi,Bahati Chihula  mkazi  wa  kijiji cha Kishinda kata ya Kamhanga wilayani Geita.

Amesema kuwa  walimpeleka Baba yao siku ya jumatano ya tarehe 5 mwezi huu kwa lengo la kupatiwa matibabu ya tezi dume lakini jambo la kusikitisha  alikutana na  huduma  zisizostahili  za wauguzi   hali  ambayo imepelekea  mzazi  wake kupoteza maisha kutokana na kukosa huduma nzuri za afya.

“Tulifukuzwa katika wodi ya wagonjwa kwa madai kuwa hatutakiwi kukaa katika wodi hiyo na tulipotoka nje baada ya dakika chache niliporudi sikumkuta mgonjwa wangu pale wodini na baada ya kuchunguza tukamkuta yupo chooni akigaa gaa na nilipouliza kwanini mgonjwa wangu yupo chooni katika hali ile   muuguzi alinijibu wewe hutakiwi kujua nenda zako. Na kutokana na huduma mbovu za hospitali hii imepelekea kuondoa uhai wa baba yangu kwani hakuwa mahututi sana na sisi kama familia hatutachukua maiti mpaka sheria ifuate mkondo wake”Alisema Bahati.

Hata hivyo mmoja kati ya wananchi  ambae ana mgonjwa anaye muuguza katika  hospitali  hiyo Felix  Joseph ameeleza  tatizo kubwa ni walinzi pamoja na wauguzi kwani  wamekuwa wakiwatusi wagonjwa na wananchi  wanaokuwa wakifika katika hosptali hiyo.

Kutokana na uzito wa swala hilo mbunge wa Geita vijijini  Joseph Msukuma amefikisha malalamiko hayo katika kikao cha sita cha kamati  ya ushauri  ya mkoa  kutaka  kujua utawala bora ukoje katika hospitali  hiyo na  juu  ya hatua zilizochukuliwa na mganga mkuu wa mkoa dhidi ya mgonjwa aliyefia chooni .
“Mwenyekiti nilikuwa nataka kuuliza kuhusiana na utawala bora kwenye hospitali ya Mkoa Jana mpiga kura wangu alimleta baba yake mzazi hospitalini hapo cha kusikitisha ni kwamba alifukuzwa na kutolewa nje, je ni haki? naomba mganga mkuu atujibu ameshachukua maamuzi gani juu ya wale ambao wameshiriki katika kitendo hicho cha unyanyasaji”aliuliza Msukuma.

Akijibu kuhusiana na tuhuma hizo za kumwacha mgonjwa  na mwisho akapoteza uhai wake, mganga mkuu wa mkoa Joseph  Kasala,amefafanua kuwa walipewa mgonjwa huyo akiwa anasumbuliwa na tezi  dume na kwamba wakati  daktari  ambae alitakiwa  kumfanyia upasuaji  alishindwa kutokana na maumivu aliyokuwa   nayo mgonjwa.

Sanjari  na hayo mkuu wa mkoa wa Geita Meja Jenerali Mstafu   Ezekiel  Kyunga amemwagiza mganga mkuu kwenda hospitalini hapo na kupata habari za kina na kujua  ni  nani  ambae amefanya  uzembe wa namna hiyo  na  kama mtu akibainika hatua   za  kisheria zitachukuliwa  dhidi  yake.

No comments