Header Ads

Uchaguzi wa Marudio Zanzibar, ACT-WAZALENDO yasema haitashiriki.

Chama cha siasa cha ACT-WAZALENDO kimepinga marudio ya uchaguzi mkuu Zanzibar uliopangwa kufanyika Machi 20 mwaka huu, na kuongeza kuwa chama hicho hakitashiriki kwenye uchaguzi huo.
Kikao cha Kamati kuu ya ACT Wazalendo Kimetoa uamuzi huo baada ya kukutana jana na kutoa wito kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuchukua hatua stahiki kwa mamlaka aliyopewa kikatiba kuhakikisha Umoja na Amani ya Taifa inaendelea kuimarika nchini, na kuongeza kuwa mkwamo wa kisiasa Zanzibar utapatikana kwa njia ya mazungumzo yatakayohusisha wadau muhimu katika mchakato wa Uchaguzi.
Akitoa maazimio ya kamati kuu ya ACT Wazalendo, kiongozi wa Chama hicho, ZITO KABWE akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es saalaam, amesema kwa sasa chama hicho kinakusudia kuondokana na siasa za matukio na vijemba na kujikita kwenye siasa ya Maendeleo .
Pia chama hicho kimeweka wazi mapato na matumizi ya fedha kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka jana kikidai kupokea na kutumia zaidi ya shilingi milion 656.6 na kuvishauri vyama vingine viweke wazi kwa umma taarifa yao ya fedha.
Katika uchaguzi mkuu wa oktoba mwaka jana, ACT-WAZALENDO ilifanikiwa kupata mbunge mmoja na madiwani 42.

No comments